ADVERT

15 August, 2008

KIZAZI CHA MAPAMBANO NA TAIFA LA MABAVU

KIZAZI CHA MAPAMBANO NA TAIFA LA MABAVU
Na Michael Dalali.

Wahenga walisha tuasa “samaki mkunje angali mbichi!” na wengine wakazidi kusisitaza “udongo ufinyange ungali maji!” na hatimaye kuhitimisha “chele chela mwana kulia, hulia mwenyewe”. Methali zote na semi zimeweza kujikita katika kusisitiza kuboresha kitu kingali mapema.

Ni takribani wiki mbili zimepita tangu kuzuke sakata la maandamano ya wanafunzi wa shule za msingi na sekondari kupinga ongezeko la nauli kwao toka Tsh 50 hadi Tsh 100! Lakini je nini hasa kitendo kama hichi kitokee katika kipindi kama hichi?historia ya maandamano na migomo ya hadharani inaashiria mwendo wa Taifa kuelekea wapi? Je kitendo hichi kimeangaliwa kwa umakini na undani stahili?

Mara kwa mara tumeshazoea kusikia migomo hasa ya wanafunzi wa vyuo ambao hugomea masuala mbali mbali kama njia mahsusi ya kushinikiza serikali kutekeleza matakwa yao ama maombi ambayo huwa kwa kipindi hicho hayapewi uzito stahili.

Ukiachilia mbali wanafunzi wa vyuo, tunaweza kuwaona tena kundi la wafanyakazi kandamizwa na waajiri kimaslahi ama wenye kuhisi hawatendewi haki kama Waalimu ambao huwa mstari wa mbele mara kwa mara kupigania haki zao mathalani kucheleweshwa kwa mishahara na uwepo wa urasimu katika kuipata.

Kundi kandamizwa jingine ni wazee wastaafu wa maofisi kadha wa kadha mathalani wazee wastaafu waliofanya kazi katika iliyokuwa jumuiya ya afrika mashariki wanavyopambana kutetea haki yao.

Migomo ni moja wapo ya zana katika kampeni hasa za ushawishi na utetezi ambazo hutumiwa kupenyeza na kuhimiza fikra fulani ambayo inahisi hitendewi haki inayostahili. Hapa tunaweza ona mifano michache kama kugomea kula chakula hususan kwa wafungwa ama wanafunzi wa shule za kulala “bweni”, kulala barabarani, kuandamana.

Historia inatufundisha hata wapambanaji wetu wa harakati za ukombozi wa bara la afrika pindi ambapo njia za kidiplomasia za kudai madai yao kutekelezwa yalipogonga ukuta nao mara kwa mara walitumia migomo kuhakikisha mahitaji yao yanafikiwa.

Tumeshawahi kufundiswa jinsi wazee wetu walivyo wagomea wakoloni kwa kuchemsha begu za mazao ambayo walitakiwa kuyapanga kama njia mahsusi ya kudhihirisha maono yao na fikra juu ya unyanyasaji na ukandamizwaji ambao serikali za kikoloni zimekuwa zikiwatendea kuelekea kudai uhuru wa nchi yao.

Migomo huwa mwanya wa kutumika kudhihirisha kuchoshwa, manyanyaso, amonevu na kuporwa haki ambayo wahusika wanadhami wanaskahili kuipata.

Si mara zote migomo imeweza kuwa suluhisho bora la mapambano ya kudai haki na ustawi toka kwa wagomaji hao ambao huwa na matarajio ya kuhimiza upatikanaji wa suluhisho la matatizo yao.

Lakini mgomo bora unapaswa uguse jamii hususan matatizo yanayowakabili na hapo ndipo utakuwa sauti yao yaani kuwa sauti ya umma na ikumbukwe sauti wa watu ni sauti ya MUNGU! “Populi voix populi Deus”.

“Kwa nini watoto wamegoma kwani wao ndiyo wanaolipa?”, “Hao lazima watakuwa wametumwa tu….!” Ni moja ya mitazamo ya wananchi ambayo waliweza toa maoni yao juu ya sakata hili.

Nani amewatuma watoto hawa? Je wao hawahisi machungu na makali ya maisha ambayo yanawakabili wananchi kila kukicha? Je si sehemu ya familia ambazo hukabiliwa na changamoto za kipato cha chini kulinganisha na mahitaji?

Hapa ndipo wanaibua maswali kadha wa kadha na kuangalia wapi hasa tulipotoka! Ya wapi mabasi ya wanafunzi ambayo yalikuwepo? Najua kwa wengine hii inaweza kuwa kauli ambayo haieleweki vichwani mwao kwani walizaliwa na kutokukuta mabasi haya.Nani aliyachukua na kuyageuza kwa manufaa binafsi?ama ndiyo “Chukua Chako Mapema”?!

Lakini je kama tunajikita katika mikakati mikubwa sana na yenye kugharimu fedha nyingi katika kujitahidi kuchochea elimu mathalani ya shule ya msingi na sekondari kwa mikakati kama ya MMEM na MMES ni vipi tunahakikisha mazingira bora yanajengwa kwa maendeleo ya elimu chini?

Je ujenzi tu wa madarasa mapya na kuongeza shule inatosha kuboresha elimu nchini? Je mazingira ya kunyanyaswa na kuonewa katika kuelekea eneo la kupata maarifa ni kusaidia ukuaji wa elimu nchini? Ni namna gani tunaongeza mvuto kwa upatikanaji wa elimu nchini?

Waswahili wanasema “simba akizidiwa na njaa hatimaye hula hata nyasi!”, je mgomo wa wanafunzi wadogo wa shule za msingi na sekondari si kikomo na njia ya kuwasilisha kiini cha matatizo waliyonayo katika upataji elimu yao? Kuwa jasiri na dhabiti kujitoa tayari kwa lolote litakalo tokea?

Uhai na ustawi wa taifa lolote huangaliwa na mbegu iliyopandikizwa katika kizazi kipya. Mfano: nchini Marekani kila kukicha wanaendelea kupandikiza dhana ya nchi yao ni taifa kubwa, tawala kidunia na jasiri kwa kizazi hata kizazi “Pax Americana” hii inajenga taifa imara kwa upande wao.

Upandikizwaji wa chuki na ubaguzi miongoni mwa taifa hususan kwa watoto na vijana ni mbegu ambayo ngumu sana kuing’oa mapema ikishamea na kustawi.Vivyo hivyo uwepo na ustawi wa taifa lenye kuwasilisha maoni na fikra zao kwa njia za ubabe na nguvu mathalani za migomo! Hili ni taifa hatari sana!!

Lakini bado tunahitaji taifa lenye ujasiri katika kusimamia misingi ambayo wanaamini ni haki yao na kuidai endapo inaporwa na si kuwa na taifa zoba! Kwa mienendo ya watoto na vijana wetu tunaweza kutabiri ni namna gani baada ya miaka kadhaa ijayo namna taifa letu litakavyo kuwa.

Wanasaikolojia wameweza kustadi na kung’amua umuhimu wa makuzi na uangalizi bora wa mtoto tangu mimba itungwe!kwani kila kitu baada ya hapo wanaamini huweza kumuathiri kwa kiasi kikubwa sana namna na miendendo ya maisha ya mtoto huyo na ndiyo maana wakajitokeza wasomi kadha wa kadha kama Erickson, Jean Piaget, walioweza kudhihirisha hili.

Hala hala mdharau mwiba wahenga walishatanabaisha kuwa guu huota tende! Huu si wakati wa kudharau namna ya uwasilishwaji wa mara kwa mara wa wananchi juu ya machungu, hali ngumu ya maisha inayowakabili kila kukicha tofauti na juhudi zao katika kupambana na maisha,Je kila kukicha askari wataendelea kutii amri huku nao wakikabiliwa na machungu na maumivu ya maisha?

0755-459 783
michaeldalali@yahoo.com

No comments: